Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2023, Abdalla Shaibu Kaim amesema mafanikio waliyoyaona katika miradi iliyopitiwa na Mwenge wa Uhuru 2023 yametokana na uongozi mahiri wa viongozi wa Wilaya hiyo huku akibainisha kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo, Esther Mahawe amemheshimisha Rais Samia Suluhu Hassan kwa usimamizi mzuri wa miradi mbalimbali.
Amesema kuwa umahiri wa usimamizi wa miradi umefanyamiradi kutokukutwa na dosari huku akweka wazi kuwa Halmashauri hiyo imeweza kutoka na ‘clean sheet’ ya kibabe.
Kaim amesema hayo wakati wa makabidhiano ya Mwenge huo kati ya Wilaya ya Mbozi na Halmashauri ya Mji Tunduma.
“Tumepitia miradi yote. Nipende tu kusema kuwa Mbozi mmetisha, Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya umetuheshimisha sana na umemheahimisha Mheshimiwa Rais Samia. Usimamizi mahiri ya miradi umewezesha Mbozi mmetoka na ‘clean sheet’ ya kibabe” amesema Kiongozi huyo wa Mbio za Mwenge kitaifa kabla Mwenge huo haujapokelewa Tunduma.
Amesema kuwa utekelezaji wa miradi kwa viwango ni njia mojawapo ya kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan hali ambayo itasaidia kupata miradi mingine.
Akizungumza katika majumuisho ya mbio hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Esther Mahawe amesema mafanikio yanayopatikana katika utekelezaji wa miradi katika Halmashauri hiyo yanatokana na ushirikiano kati ya wafanyakazi wa Wilaya hiyo na wananchi.
“Tunashukuru sana miradi yetu yote imezinduliwa na kuwekwa mawe ya msingi. Mafanikio haya yanatokana na ushirikiano tulionao katika Wilaya yetu” ameeleza Mkuu huyo wa Wilaya.
Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani Mbozi ulitembelea miradi nane yenye thamani ya Sh8.2 bilioni huku ukikimbizwa Kilometa 130 katika Wilaya hiyo.
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa