Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Abdallah Nandonde amepiga marufuku tozo ya asilimia kumi inayochajiwa na wenyeviti wa vijiji na watendaji wakati yanapofanyika mauziano ya viwanja au nyumba katika halmashauri hiyo.
Agizo hilo amelitoa leo Jumatatu July 31, 2023 wakati akifungua mafunzo ya Mfumo wa Uhasibu na Utoaji Taarifa za Fedha kwa Ngazi ya Kituo cha Kutolea Huduma (FFARS) kwa watendaji na baadhi ya watumishi katika Halmashauri hiyo.
Mafunzo hayo ya FFARS yatasaidia mambo mbalimbali ikiwemo kudhibiti fedha zinazotolewa na wadau au Serikali ili zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa katika kutoa huduma bora kwa wananchi au jamii kwa ujumla.
Mkurugenzi huyo amesema asilimia hizo wanazotoza watendaji na wenyeviti hazipo kisheria huku akihoji wanakozipeleka.
"Niwapeni angalizo, unakuta watu wanauziana shamba au nyumba unachaji asilimia 10 unaipeleka wapi na unakatia risiti gani?" amehoji
"Wakati wananchi wanauziana shamba halafu wewe unataka asilimia 10 huoni kuwa unamuumiza mwananchi? Hiyo ni rushwa. Sasa kuanzia leo hicho kitu tuache. Tunaidhalilisha Serikali" amesisitiza.
Akizungumza katika mafunzo hayo mkurugenzi huyo amesema mafunzo hayo yatasaidia kutambua mapato na matumizi kupitia mfumo kwa urahisi.
"Baada ya mafunzo haya washiriki wataweza kuandaa malipo yote kupitia mfumo"
Pia, Mkurugenzi huyo amewaonya watumishi hao kuwa wasitumie steshenari kutokana na unyeti wa taarifa zitakazokuwemo katika mfumo huo.
"Tusije kwenda kufanya kazi hizo katika steshenari, kila kitu kinachofanyika katika serikali ni siri, tukienda katika steshenari zile usiri unakuwa hakuna tena" amesema na kuongeza;
"Lakini pia tukitumia mfumo huu utatusaidia kutambua wadau waliochangia fedha katika miradi ya maendeleo tofauti na ilivyo sasa tunapokea fedha bila kufahamu ni mdau gani ameleta fedha hizo" amesema
Ameeleza kuwa hiyo itasaidia kujua mapato katika kila chanzo ikiwemo michango ya maendeleo ambayo ni lazima iingizwe benki
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa