Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa ana Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt Charles Mahera ametoa maagizo kwa watumishi wa afya katika Mkoa wa Songwe ambayo yatasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi wa mkoa huo.
Akizungumza na watumishi hao leo Alhamisi Julai 13, 2023 katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Dkt Mahera amesema kuwa lengo la Tamisemi ni kutoa huduma bora hivyo amewaagiza watumishi na viongozi katika sekta ya afya kuzingatia utawala bora.
“Sisi Tamisemi katika kitengo cha Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe tuna mpango mkakati kuanzia mwaka 2022/23 hadi 2025/26 wa kuchochea masuala ya utawala bora na ushirikishwaji wa jamii katika mfumo wa utawala. Ninyi kama viongozi mnatakiwa muwe na skills za leadership ndio maana tunatoa semina ili mtusaidie kutoa hizo huduma nzuri” amesema.
Naibu Katibu Mkuu huyo amesema kuwa jambo la pili ni kuhakikisha wananchi wengi wanapata huduma bora katika ngazi za chini katika maeneo yao.
“Tunataka watu wengi kwenye primary health ambazo ni zaidi ya Watanzania asilimia 80 hadi 90 ya Watanzania wanatibiwa. Ndio maana mnaona vituo na zahanati vimeshushwa huko chini na Serikali itaendelea kujenga na kuboresha vituo hivyo sasa tunawategemea ninyi zaidi” ameeleza
Amesema kuwa Serikali inapotimiza wajibu wake wa ujenzi wa vituo na kuboresha miundombinu inawategemea watumishi hao kusaidia kutoa huduma bora.
Jambo lingine ambalo Dk Mahere amewaagiza watumishi hao ni suala la mawasilano ambapo amewataka kutathimini namna wanavuyowasiliana na wagonywa au viongozi wanavyowasiliana na watumishi hao.
“Lakini tuna mifumo mingi ya Tehama tunataka itumike itusaidie kukusanya takwimu. Mhakikishe mnaweka kwenye mifumo takwimu sahihi na kwa wakati ili ziweze kuwasaidia kufanya mipangio vizuri” amesema
Amesema kuwa watumishi hao wanatakiwa kufanya tafiti mbalimbali huku viongozi wakitakiwa kusimamia vizuri watumishi wa kada hiyo ili kufikia matarajio ya viongozi wa kitaifa.
Aidha, Dk Mahera amesema kuwa Serikali inaendelea kutoa fedha katika sekta ya Afya ili kuweka mazingira bora ya kutoa huduma za kitabibu ambapo mkoa huo umepewa shilingi bilioni 5.4 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya afya katika halmashauri za mkoa wa Songwe.
“Msimamie vizuri fedha hizi zinazoletwa kwenu isiwe kama ni fursa ya kuweza kupiga. Masuala ya upigaji yamepitwa na wakati. Ukipiga utaumia. Mfanye matumizi mazuri ya dawa kwa sababu fedha nyingi zimeelekezwa huko kwa hiyo hakikisheni dawa zinawafikia walengwa” amesisitiza
Pia, Dk Mahera amesema kuwa Serikali inaendelea kuboresha masuala ya usafiri ambapo kila halmashauri itapewa magari matatu ikiwemo mawili ya kubebea wagonjwa.
“Tunaendelea kuboresha masuala ya usafiri ili watu wetu wale walioshindikana kutibiwa katika sehemu moja wapelekwe kwenye eneo jingine. Kuna magri 528 yanakuja, katika hayo ambulance zipo 316 hizi tutagawa katika kila halmashauri ambulance mbilimbili na hardtop mojamoja” amesema
Hata hivyo, Dk Mahera amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Abdallah Nandonde kuwasimamisha kazi Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Mbozi, Mganga Mfawidhi na Mfamasia ili kupisha uchunguzi wa mapungufu yaliyobainika katika hospitali hiyo.
“Watu watatu hao wasimamishwe, uchunguzi ufanyike ndani ya muda mfupi tupate taarifa. Tunaposema tunakusimamisha hatujasema tunakufukuza kazi, tunapomsimamisha isichukue muda mrefu. Ufanyike uchunguzi wa haraka ili mtu aweze kupata stahiki yake. Fanyeni uchunguzi wa haraka bila upendeleo” amesema.
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa huo, Happiness Seneda amesema kuwa amepokea maelekeza hayo na kuahidi kuwa atakwenda kuyafanyia kazi na kuyasimamia.
“Tutakwenda kufanya mabadiliko makubwa katika sekta hii. Watumishi nitawahamisha na nitawababilisha wa huku atakwenda huko lakini tutachunguza tukibaini umefanya ubadhirifu tutakufukuza kazi” ametahadharisha
Amesema kuwa watashirikiana na vyombo vya dola kuhakikisha wanabaini wizi wa dawa na vifaa tiba katika hospitali na vituo vya afya.
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa