Mkuu wa Wilaya ya Mbozi mkoni Songwe, Esther Mahawe amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa wahudumu wa afya watakaopita katika maeneo yao kutoa chanjo ya ugonjwa wa Polio huku akiwashauri wananchi wa Wilaya hiyo kupuuza baadhi ya watu wanaopotosha juu ya chanjo hiyo.
Mkuu huyo wa Wilaya ametoa rai hiyo leo Jumanne Septemba 12, 2023 baada ya unzinduzi wa chanjo ya Polio awamu ya pili katika Wilaya hiyo ambapo amesema wapo baadhi ya watu wanapotosha juu ya mambo yanayofanywa na Serikali hivyo wananchi wachukue tahadhari.
Amesema kuwa ugonjwa huo ambao hauna tiba ni hatari kwa watoto chini ya miaka nane hivyo wazazi na walezi wahakikishe watoto wao wanapata chanjo hiyo itakayowazuia na maambukizi ya ugonjwa huo kwa kuwa chanjo hiyo haina madhara.
“Niendelee kuomba wananchi wote wanapotembelewa majumbani na wataalamu wetu wa afya watoe ushirikiano ili waweze kupatiwa elimu hii” ameeleza
“Leo katika uzinduzi tumekuwa na wakuu wa idara za shule za msingi na viongozi wa dini, nimeomba sana watu hao watusaidie kwasababu wanakutana na makundi mengi ya watu” amesema
Amesema kuwa wamekubaliana na viongozi wa dini wawaruhusu wataalamu wa afya kutoa elimu kwenye nyumba za ibada ikiwemo makanisani na misikitini ili elimu hiyo kuweza kuwafikia walio wengi.
DC Mahawe ameeleza kuwa athari ya ugonjwa huo ni pamoja na kusababisha ulemavu wa kudumu pale unapompata mtu.
“Ugonjwa huyu unasababisha ulemavu wa kudumu tangu kuambukizwa hadi kifo hivyo ni vizuri tukachukua tahadhari kabla ya hatari. Niwaombe wananchi wa wilaya ya Mbozi wote tuepuke wale watu watakaokuja na upotoshaji wakati watu wa afya wakiwa wanapita kutoa elimu hizi una watu wanapenda kupotosha jamii mambo mazuri yanayofanywa na Serikali ” ameeleza
Amesema kuwa wananchi wanapaswa kuchukua tahadhari kwa kuwa tayari mgonjwa mmoja amegundulika kuwa na polio katika mkoa wa Rukwa.
“Rukwa ni mkoa jirani na sisi kwa hiyo tuchukue tahadhari na sisi hatuko salama na sisi hatuishi kisiwani ni Imani yangu wananchi wa Wilaya ya Mbozi watachukua tahadhari” amesisitiza
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa