Mbozi. Ikiwa anatimiza miaka miwili madarakani, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amedhihirisha utendaji wake katika miradi mbalimbali nchini.
Tangu aapishwe Machi 19, 2021 kushika wadhifa huo amekuwa akifanya jitihada za kuanzisha na kuendeleza miradi mikubwa ya maendeleo kwa lengo la kukuza uchumi katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Kama ilivyo katika maeneo mengine, mafanikio yamejidhihirisha katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe ambayo imenufaika na miradi mbalimbali ya maendeleo kwa kipindi cha miaka miwili ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Mkuu huyo wa nchi ambaye ameandika historia ya kuwa Rais wa kwanza mwanamke Tanzania, ameandika historia katika miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Mbozi.
Miongoni mwa mafanikio ambayo yamepatikana ndani ya kipindi cha uongozi wake Rais Samia ni pamoja na sekta ya Afya, Elimu, Miundombinu, Kilimo na Maji.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Bw. Abdallah Nandonde anaeleza kuwa, Kati ya Julai 2020 hadi kufikia mwezi Januari 2023, jumla ya Tshs. Bilioni 16 zimepokelewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambapo kati ya fedha hizo kiasi cha shilingi bilioni 5.6 ni fedha za ndani (Ruzuku ya Serikali Kuu) na shilingi bilioni 10.3 ni fedha za wafadhili.
“Ni katika kipindi cha miaka miwili ya uongozi wa Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia ndipo ujenzi wa vituo vya afya vipya vitatu vimejengwa katika wilaya hiyo ambavyo vinagharimu shilingi billion 1.3 ambavyo ni Itaka, Nambinzo na Hezya” anafafanua Bw Nandonde
Vituo hivyo vitaleta ahueni ya upatikanaji wa huduma za afya kwa wakazi wa wilaya hiyo.
Pia, shilingi milioni 500 zimetolewa kwaajili ya ukamilishaji wa Zahanati 10 ambazo ni Chizumbi, Shititi, Lusungo, Nsenga, Shilanga, Mbimba, Ipanzya, Mtunduru, Isowezya na Maninga.
Katika uongozi wake Rais Samia ambaye kabla ya kuapishwa kushika nafasi hiyo ya juu nchini alikuwa Makamu wa Rais, Serikali yake imefanikisha ujenzi wa shule mpya mbili mpya za Sekondari zenye thamani ya shilingi milioni 940 kupitia mpango wa SEQUIP. Aidha matundu ya vyoo 26 vya wanafunzi kwa Shule za Sekondari Mlowo na Ilolo yamejengwa kwa thamani ya shilingi 26.4 milioni.
Pia Mama samia amejenga madarasa 146 na samani katika shule 44 za Sekondari zenye thamani ya shilingi bilioni 2.8 kupitia fedha za Mpango wa maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO-19, vilevile ujenzi wa Bweni la wanafunzi wenye mahitaji maalum Shule ya Msingi Lutumbi uliogharimu shilingi milioni 80, na pia ujenzi wa madarasa 37 na matundu ya vyoo 271 katika Shule 38 yenye Zaidi ya thamani ya shilingi milioni 904
Pia, kipindi cha miaka miwili cha serikali ya awamu ya sita wananchi wamenufaika kupitia mikopo ya asilimia 10 zinazotolewa na serikali kiasi cha Zaidi ya bilioni 1.2 kwa vikundi 213 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Hata hivyo baadhi ya miradi inayotekelezwa kwa fedha za mapato ya ndani ni pamoja na ununuzi wa mtambo wa barabara wenye thamani ya milioni 500, ukamilishaji wa Kituo cha Afya Halungu milioni 400, ukamilishaji wa zahanati ya Mbimba na Nambala milioni 40, kuwezesha ujenzi wa maegesho ya magari Vwawa milioni 74, ununuzi wa mashine ya kufyatua tofali milioni 29.7.
Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri George Musyani amesema kuwa halmashauri hiyo inampango wa kununua mitambo mingine ya kutengenezea barabara inayofanya kazi sambamba na mtambo huo.
‘’Kupitia mapato ya ndani halmashauri yetu inampango wa kuongeza mitambo mingine inayofanyakazi sambambamba na mtambo huo ’’ alisema Musyani
Ili kuimarisha sekta ya kilimo katika Wilaya ya Mbozi, Machi 10, 2023 Serikali inayoongozwa na Rais Samia imegawa pikipiki 81 kwa maofisa ugani wa Wilaya hiyo.
Katika ugawaji wa pikipiki hizo, Mkuu wa Wilaya hiyo, Esther Mahawe alisema amesema kuwa wilaya ya hiyo inakwenda kufanya mapinduzi makubwa katika sekta ya kilimo baada ya maafisa ugani kukabidhiwa pikipiki na Serikali.
DC Mahawe alisema anaamini kama wilaya inakwenda kuzalisha kwa wingi kutokana na wataalamu wa kilimo kuwezeshwa vitendea kazi ambavyo vitawafanya wamfikie mpaka mkulima wa chini huku alimpongeza Rais Samia kwa kuwapatia vyombo hivyo ambavyo vitakwenda kuinua utendaji wa maofisa hao.
"Hata kama watu wanasema hawajaona kama vitu vinafanyika, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni mama anaupiga mwingi mpaka unamwagika" alisema DC huyo na kuongeza
Tumeona kwa macho yetu juhudi za mama kwaajili ya kuwezeshwa kilimo cha kisasa chini ya Waziri wake wa Kilimo, Bashe. Niwahimize muende mkafanye kazi ndugu zangu mkaoneshe kabla ya kupata pikipiki ilikuaje na baada ya kupata imekuaje" alisema
Akiwa kwenye ziara katika Wilaya ya Mbozi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Kassim Majaliwa Majaliwa alibainisha kuwa
ili kuwapa motisha wakulima wakiwamo wa Wilaya hiyo, Serikali imetoa ruzuku kwenye pembejeo za kilimo ikiwemo mbolea hali ambayo itawasaidia wananchi wakowemo wa Wilaya ya Mbozi wapate pembejeo kwa urahisi.
Waziri Mkuu huyo aliwasisitiza wananchi wa Mbozi kulima zao la kahawa kwa kuwa zao hilo ni la mkakati na muhimu
Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi katika kipindi cha Uongozi wa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepata mafanikio makubwa hususani katika Nyanja za Sekta ya Elimu, Afya na uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF III) na ukusanyaji wa mapato ya ndani ambapo asilimia 40 ya fedha za makusanyo imekuwa ikipelekewa kwenye kuchangia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo utoaji wa mikopo kwa Vikundi vya akina mama, Vijana na watu wenye Ulemavu.
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa