Mbozi. Kamati ya kudumu ya bunge ya masuala ya Ukimwi, kifua Kikuu, Dawa za Kulevya imeridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe ambapo kitengo cha mionzi katika hospitali hiyo kinatarajiwa kuanza kutoa huduma mwezi Mei mwaka huu.
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe inajengwa katika Kijiji cha Hasamba Kata ya Vwawa wilayani Mbozi ambapo mradi huo unatarajiwa kuwa na majengo 14.
Hadi sasa ujenzi wa mradi huo umetumia jumla ya Sh16.3 bilioni ambapo Sh13.1 bilioni ni kwaajili ya ujenzi na Sh3.2 bilioni ni kwaajili ya ununuzi wa vifaa tiba kupitia fedha za Uviko-19.
Akizungumza leo Ijumaa Machi 17, 2023 wakati wa kikao cha majumuisho baada ya kamati hiyo kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyotengewa fedha kwa mwaka fedha 2022/23 katika Mkoa wa Songwe, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Stanslaus Nyongo amesema kuwa kamati yake imeridhishwa na maendeleo ya mradi huo.
"Kamati inawapongeza na imeridhishwa na ujenzi wa mradi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe kwa namna inavyoendelea na wamejikomiti kuwa huduma ya miaonzi yataanza kutoa huduma kuanzia mwezi Mei mwaka huu" amesema Nyongo kwa niaba ya kamati hiyo.
Kamati hiyo imewashukuru viongozi wa mkoa wa Songwe kwa kushirikiana na Wizara ya Afya katika utekelezaji wa miradi hiyo.
"Ninawashukuru sana viongozi wa Mkoa wa Songwe kwa ushirikiano mkubwa na Wizara ya Afya maana maeneo maeneo mengine viongozi wanawaachia usimamizi wa ujenzi Wizara ya Afya hivyo kwa Mkoa huu naona mnaou-own mradi" amesema
Pia, Kamati hiyo imefanya ukaguzi wa shughuli za utoaji wa huduma za ushauri nasaha, upimaji wa virusi vya Ukimwi, matumizi ya dawa za kurefusha maisha, ikiwemo kutembelea vituo vya kutolea huduma hizo mkoani hapo ambapo iliishauri Wizara ya Afya kuharakisha mpango wa kuwasajili kwa njia ya kielekroniki (alama za vidole) watu wote wanaotumia dawa za kufubaza virusi vya Ukimwi (ARV) kupitia kliniki ya matunzo na tiba (CTC), ili kuwa na mfumo mmoja wa utambuzi, utakaosaidia kujua idadi halisi ya watu wote wanaotumia dawa hizo hapa nchini.
Nyongo amesema mfumo huo wa usajili kwa njia ya kielektroniki utasaidia Taifa kuwa na mfumo mmoja wa utambuzi wa watu (wateja) wote wanaotumia dawa hizo za kurefusha maisha (ARV), lakini pia utasaidia kuondoa mkanganyiko wa taarifa.
“Ushauri uliotolewa na wabunge ni mzuri sana kwani tukiwa na mfumo mmoja wa utambuzi wa watu wanaotumia dawa utasaidia kumaliza mamalalamiko ya (utoro) kwa wateja wanaotumia dawa hizo za kurefusha maisha (ARV) katika baadhi ya vituo” amebainisha Nyongo.
Kwa upende wake Meneja wa Mpango wa Taifa wa kudhibiti Ukimwi kutoka Wizara ya Afya, Dk Anath Rwebembera amesema kuwa Wizara ina mpango wa kusajili watu wanaotumia dawa za kufubaza virusi vya Ukimwi kwa kuichukua alama za vidole ili kuepuka mkangayiko wa taarifa kwa mteja huyo akihama kutoka eneo moja kwenda kingine.
Amesema tayari Wizara ya Afya imeanza utekelezaji wa mpango huo kwa kuanza majaribio kwenye mikoa mitatu ya Dar es salaam (Kigamboni), Pwani na Morogoro.
Amesema mpango huo wa majaribio unatarajia kumalizika hivi karibuni na ukionyesha mafanikio utaanza kutekelezwa kote nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS), Dk Leonard Maboko amewashukuru wajumbe wa kamati hiyo kwa maoni yao huku akibainisha kuwa takwimu za watu wanaoacha kutumia dawa za kufubaza maambukizi ya Ukimi zinazidi kupungua kutokana na wafanyakazi kuweka mkazo hata kufanya kazi zaidi ya masaa ya kazi.
"Niwaombe wabunge kutumia platfom yao kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kupima ili kujitambu" ameshauri.
Naye Katibu Tawala Mkoa wa Songwe (RAS), Happiness Seneda ameishukuru kamati hiyo kwa kutembelea miradi ya mkoa huo huku akitoa rai kwa kamati na Bunge kuungalia mkoa huo kwa jicho la kipekee kutokana na mkoa huo kuwa mchanga.
"Sisi Songwe ni Mkoa mchanga naamini mtatuangalia kwa jicho la tofauti kutokana na uchanga wake,
Tutakuwa wachoyo wa fadhila tusipoishukuru Serikali kwa kutuletea fedha na tunashirikiana vizuri na wizara sehemu yenye changamoto tunazitatua" amesema RAS huyo.
Amewakaribisha wabunge hao katika mkoa huo kutumia fursa za kilimo, biashara na uanzishwaji wa viwanda kutokana na mkoa huo kuwa na malighafi nyingi za shambani.
Mbozi
Anuani: 3
Simu: 025-2580272
Simu ya kiganjani:
Barua pepe: ded@mbozidc.go.tz
Hati Miliki 2017 Halmashauri ya Wilaya-Mbozi. Haki zote zimehifadhiwa